Monday, August 21, 2017

HASSAN MAAJAR TRUST YAKABIDHI VITABU VYA KUSOMEA KATIKA SHULE YA SHIMBWE, KILIMANJARO





Makamu Mwenyekiti wa Hassan Maajar Trust - Sharif Maajar akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe, Anne E Mghwira.



HOTUBA FUPI YA MAKAMU MWENYEKITI WA HMT KATIKA HAFLA SHULE YA SEKONDARI SHIMBWE – TAREHE 19 AGOSTI, 2017
Niko hapa kuwakilisha Hassan Maajar Trust, kwa kifupi, HMT; taasisi ambayo ilianzishwa mwaka 2011 kwa lengo kuu la kuchangia elimu bora katika shule nchini Tanzania. Mimi ni Makamu Mwenyekiti wa HMT. Ili kutimiza lengo hilo, tumekwa na mipango na miradi mbalimbali ya kuboresha mazingira ya kusomea na kufundishia.
Uhusiano wetu na shule hii ya Shimbwe Sekondari ni wa kipekee kabisa. Uwepo wetu hapa leo, ni mwendelezo wa historia yetu na shule hii ambayo ilianza wakati wa ujenzi wake miaka ya 70.
Wakati huo, Mwenyekiti wa HMT, Balozi Mwanaidi Sinare Maajar, alitumia likizo zake kujiunga na Wanafunzi wenzake kutoka shule mbalimbali kushiriki kufytua matofali ya kwanza yaliyojenga shule hii.
Huu ulikuwa ni mwanzo wa safari endelevu ya kuchangia na kurejesha kwenye jamii na hususan hapa Shimbwe Sekondari. Nasema hivyo kwa sababu, baada ya hapo, popote alipokuwa Balozi Maajar alitafuta misaada kuendeleza miundombinu na taaluma kwa ajili ya shule hii.
Juhudi hizi zilichukuwa kasi mpya baada ya kuanzishwa kwa Taasis ya Hassan Maajar Trust. Kupitia HMT, tuliweza kuwatambulisha mashirika mawili ya Kimarekani; Malaika Kids na Powering Potential ambao kwa kushirikiana na nasi walifadhili kitengo cha compyta hapa shuleni.  Malaika Kids walitoa laptop 10 na Powering Potential wakaweka programu maalumu ya kufundishia iitwayo ‘Rachel’ pamoja na kutoa mafunzo waalimu wa ICT.
HMT kwa upande wake iligharamia utengenezaji wa samani (meza 13 na viti 60) kwa ajili ya chumba cha compyuta.
Aidha, HMT iliwashirikisha, Vodacom Foundation nao wakatoa laptops 10 na compyuta 10 pamoja na mafunzo maalum kwa waalimu.
Tunaamini ni kwa historia hiyo ya kujivunia, ndiyo imepelekea uongozi wa shule kutujulisha na kutualika tushiriki hafla hii ya ufunguzi wa bweni. Nasi katika HMT tumeona ni heshma kubwa kwa taasisi yetu, hivyo tumeamua tusije mikono mitupu.
Tumeona pia kati ya mambo yanayoweza kuchangia elimu bora ni kujenga utamaduni wa kujisomea. Hivyo basi tumeleta vitabu kwa ajili ya kujisomea.
Kwa niaba ya Bodi ya Hassan Maajar Trust, naomba kuwasilisha mchango wetu huo.




















No comments: